KIONGOZI WA VITENDO, MZALENDO NA MPENDA MAENDELEO

Daima tutakukumbuka Prof. Damian Gabagambi

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mnamo tarehe 18. Machi 2018 alimteua Prof. Damian Gabagambi kuwa Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC).  Akitokea Chuo cha Kilimo Sokoine (SUA), Morogoro. Toka kuteuliwa kwake Prof. Damian Gabagambi amekuwa kiongozi wa mfano katika kutekeleza majukumu ya NDC kwa weledi na ufanisi mkubwa akitamani kuiona NDC kama mkono wa uwekezaji wa Serikali ikifanikisha azma ya Tanzania ya Viwanda; hakika alipenda kuiona NDC mpya iliyojaa ubunifu.

Wakati wa utumishi wake akiwa NDC, Prof. Damian Gabagambi alisimamia kwa nguvu zote na kutekeleza miradi mbalimbali ya kimkakati ambayo ndio dhima kuu ya Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC).

Miradi hiyo ya kimkakati ni pamoja na Mchuchuma na Liganga uliopo Ludewa Mkoani Njombe, Makaa ya Mawe Ngaka yaliyopo mkoa Ruvuma, Magadi Soda, Engaruka  mkoa wa Arusha. Miradi hiyo ni kichocheo kikubwa kwa maendeleo ya viwanda nchini.

 

Pia, Prof. Damian Gabagambi alifanya kazi kwa juhudi bila kuchoka na mara zote alipenda kutuasa kufanya kazi kwa bidii huku tukitanguliza maslahi ya Shirika na Taifa mbele. Daima atakumbukwa kwa kutuachia Mpango Mkakati wa Shirika wa miaka 5 (5 Years Strategic Plan). Kwa hakika kiu na maono yake ya kutaka kupeleka jembe la mkono makumbusho ilikua ni kubwa na hili limethibitika kwani, Mpango huu chini ya uongozi wake umewezesha matrekta kupatikana kwa bei nafuu na kusambazwa sehemu mbalimbali nchini.

 

Miradi mingine iliyotekelezwa katika Shirika kwa ufanisi chini ya uongozi wa Prof. Damian Gabagambi ni pamoja na ujenzi wa miundombinu katika Maeneo Maalum ya Viwanda (Industrial Parks), ikiwemo TAMCO Kibaha. Vilevile  kuendeleza mashamba makubwa ya kuzalisha malighafi za viwanda na usindikaji na juhudi mbalimbali za kufufua kiwanda cha matairi cha General Tyre kilichopo Mkoani Arusha.

 

Prof. Damian Gabagambi alikuwa na maono ya kuhakikisha kiwanda cha KMTC kinaboreshwa na kuwa na uwezo wa kuzalisha vipuri kwa ajili ya matumizi ya mashine na mitambo mbalimbali kwa lengo la kuongeza tija katika Sekta ya Viwanda nchini ikiwa ni pamoja na kuokoa matumizi ya fedha za kigeni.

 Prof. Damian Gabagambi alitumia muda wake mwingi katika kuwaendeleza na kuwajengea wafanyakazi ujuzi ili waweze kumudu na kutekeleza majukumu ya NDC kwa ufanisi mkubwa. Hakika alikuwa Kiongozi wa Vitendo, Mnyenyekevu, Mwenye Kupenda Watu, Mchapakazi, Mzalendo na hivyo kuwa mfano wa kuigwa kwa Shirika na Taifa.

Kuondoka kwake kumeacha pengo kubwa lakini pia kuna mengi ya kujifunza kutokana na kazi zake. Ingawa hatutakua naye kimwili, daima ataendelea kuishi  kwenye mioyo yetu.

 

 BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA JINA LAKE LIHIMIDIWE.