Magari yaanza kuunganishwa Eneo la Viwanda TAMCO

Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), Prof. Damian Gabagambi amefanya ziara ya kikazi kiwanda cha kuunganisha magari cha GFA Assemblers kilichopo kibaha mkoani Pwani na kujionea kazi nzuri inayofanywa na kiwanda hicho kipya.

Katika ziara hiyo, amefurahishwa na karidhishwa na GFA Assemblers kwa kuunganisha magari hapa nchini. Nae Meneja Mkuu wa Kiwanda hicho, Ndg. Ezra Mereng amesema kuwa kwa sasa wanaunganisha magari aina ya FAW lakini malengo yao ni kuunganisha magari mengi ya kampuni mbalimbali ili kuendana na ushindani wa soko.

Wakiwa wameanza kazi ya kuunganisha magari wiki moja iliyopita, kiwanda hicho kimeshapata oda ya  magari 10 kutoka hapa nchini ikiwa ni mafanikio makubwa kwa kiwanda hicho. “Tumeanza kuunganisha magari wiki moja iliyopita na tayari tumeshapata oda ya magari 10,” amesema Bw. Mereng, Meneja Mkuu wa kiwanda hicho.

Gari zinazo unganishwa kiwandani hapo hupitia hatua 9 ndani ya eneo la uunganishaji na hatua ya mwisho uhusisha upimaji wa ubora wa gari ikiwemo kuangalia uwezo wa breki, ufanyaji kazi wa mfumo wa umeme wa gari pamoja na makosa ya kiufundi ambayo yangeweza kutokea wakati wa uunganishaji wa gari.

Magari hayo huunganishwa na Watanzania ambao wamepata ujuzi hapa nchini ikiwa ni jitihada za kukabiliana na suala la ukosefu wa ajira hapa nchini. Mpaka sasa kiwanda hicho kimetoa ajira za moja kwa moja kwa Watanzania 70 huku lengo likiwa ni kuongeza ajira kwa Watanzania wengi zaidi siku za usoni.

Nae Mkurugenzi Mwendeshaji wa NDC, Prof. Damian Gabagambi amewapongeza wafanyakazi wa kiwanda hicho  na kuwasihi kufanya kazi kwa bidii ili kujenga uchumi wa taifa, “nawasihi mfanye kazi kwa bidii kwani kazi ndio msingi wa maendeleo kwa taifa,” amesema Prof. Gabagambi. Pia amekipongeza kiwanda hicho kwa maono yao ya kuunganisha magari makubwa kwani kwa sasa taifa lina miradi mingi ya kimaendeleo inayohusisha ujenzi hivyo magari hayo yatapunguza uagizwaji wa magari kutoka nje ya nchi.

“Niwapongeze kwa kulenga muda muafaka wa kuzalisha magari haya kwani kwa sasa sekta kubwa ni sekta ya ujenzi, hivyo kuna uhitaji mkubwa wa magari haya,” amesema Prof. Gabagambi.

Kwa siku za usoni, kiwanda hiki kitakuwa ni chachu kwa kiwanda cha KMTC kilichopo mkoani Kilimanjaro ambacho ni mahususi kwa ajili ya kuzalisha vipuri vya mashine na mitambo mbalimbali kwani kitasaidia kiwanda cha KMTC kupata soko la vipuri vyake na kusaidia kujenga uchumi wa ndani kwa kutumia malighafi zinazo zalishwa hapa hapa nchini.

Kiwanda cha GFA Assemblers kimejengwa kwenye Eneo la Uwekezaji la TAMCO lililopo Kibaha, mkoani Pwani, eneo hilo linamilikiwa na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) likiwa ni mahususi kwa ajili ya uwekezaji katika Sekta ya Viwanda vya aina mbalimbali.

Kwa sasa eneo hilo lenye ukubwa wa hekari 201.63 lina kiwanda cha Kuzalisha Viuadudu mahususi kwa ajili ya Kuangamiza Mazalia ya mbu, Tanzania Biotech Products Limited (TBPL), Kiwanda cha Kuzalisha Vifungashio vya Mazao, Global Packaging Tanzania Limited (GPTL), Kiwanda cha Kuzalisha Chanjo za Wanyama, Heister BioScience, Kiwanda cha Kuunganisha Matrekta aina ya URSUS.

Mbali na eneo la TAMCO, NDC inamiliki maeneo mengine ya uwekezaji yaliyopo Tanga - kange Industrial Estate lenye ukubwa wa hekari 22.4, Kilimanjaro - KMTC Industrial Estate lenye ukubwa wa hekari 229.13, Mwanza - Nyanza Industrial Estate lenye ukubwa wa hekari 11.

Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) ni shirika linalomilikiwa na Serikali kwa asilimia 100. lilianzishawa mara ya kwanza mwaka 1965 kwa tamko la Rais yaani (The Presidential Order Number 5 of 1964) kuchukua majukumu na shughuli za lililokuwa Shirika la Maendeleo la Tanganyika, yaani, “the Tanganyika Development Corporation.”