MKURUGENZI MPYA NDC AWATAKA WAFANYAKAZI KUJITUMA

Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), Dkt Nicolaus Shombe amewataka wafanyakazi wa shirika hilo kuhakikisha wanashirikiana katika kufanya kazi kwa juhudi na maarifa ili kuhakikisha wanafikia ndoto ya shirika ya kuwa shirika bora  na la mfano kwa kutekeleza miradi mbalimbali ya kimkakati ya serikali  pamoja na kushirikiana na sekta binafsi katika kukuza sekta ya viwanda hapa nchini.

Dkt Shombe ameyasema hayo mara baada ya kuwasili rasmi katika ofisi za Makao Makuu ya NDC na kuanza kazi ambapo mara baada ya kuwasili alianza kwa kuzungumza na wafanyakazi wote wa shirika hilo ikiwa ni siku chache tangu ateuliwe na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa, Samia Suluhu Hassan kushika nafasi ya kuliongoza shirika hilo.

Akiongea na wafanyakazi wa NDC Dkt Shombe amewataka wafanyakazi hao kufanya kazi kwa bidii na maarifa badala ya kufanya kazi kwa mazoea pamoja na kutoa ushirikiano ili kuendana na kasi ya serikali ya Awamu ya sita kupitia kauli mbiu ya Kazi iendelee.

“Ninawaombeni sana ushirikiano wenu tukiwa kama familia moja, tushirikiane pamoja katika kuhakikisha Shirika linasonga mbele. Tukishirikiana tutaweza kuzitatua changamoto mbalimbali zinazotukabili kwa pamoja kutumia fursa tulizonazo nitahakikisha tunatenge muda maalum ambao tutakuwa tunakutana na menejimenti,wakuu wa Idara pamoja na wafanyakazi wote ili kusiwe na utofauti mkubwa baina ya viongozi pamoja na watumishi wa kawaida lengo likiwa ni kujenga teamwork ” Alisema Dkt Shombe.

Hata hivyo katika kuonyesha kuwa amedhamiria kubadilisha utendaji kazi wa Taasisi katika kikao hicho Dkt Shombe aliwataka wafanyakazi kuainisha changamoto mbalimbali zinazowakabili katika utendaji wao wa kazi ambapo mara baada ya kupokea changamoto hizo amehaidi kuzitendea kazi mara moja huku akiwataka wafanyakazi kubainisha fursa wanazoziona na mikakati ya kuzitumia kwa maendeleo ya viwanda nchini.

Kwa upande wake aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa NDC,ambaye kwa sasa ni Mkurugenzi wa Fedha  Rhobi Sattima alimpongeza Dkt Shombe kwa kuaminiwa na Rais na kuteuliwa kuwa Mkurugenzi Mwendeshaji wa NDC huku akisema kuwa ana imani ataifanyia makubwa NDC.

“Mkurugenzi ninakumbuka siku moja wakati uko Hazina kama Kamishina wa Mipango ulitusaidia sana katika kuhakikisha kuwa taasisi inawezeshwa kifedha na nadhani ulifanyika kuwa kama malaika kwani hatimaye leo umeteuliwa rasmi kuwa Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika Hongera sana kwani tunamatumaini makubwa na ujio wako”Alisema Bi Rhobi Sattima.

Ujio wa Dkt Shombe kuwa Mkurugenzi mpya wa NDC umepokelewa vizuri na wafanyakazi ambao wamehaidi kumpa ushirikiano wa kutosha ili kuhakikisha anatimiza adhima ya shirika hilo ya kuwa  bora na imara hapa nchini  litakalokuwa linaongoza  katika ujenzi wa Tanzania ya viwanda pamoja na kuvutia na kujenga mazingira bora wezeshi kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi.

Uteuzi wa Dkt Shombe kushika nafasi ya Mkurugenzi Mwendeshaji wa NDC na Rais umefanyika mara baada ya kufariki Dunia kwa aliyekuwa Mkurugenzi wa NDC Prof Damiani Gabagambi ambaye alifariki dunia Mwishoni mwa mwaka jana ambapo kabla ya kuteuliwa na Rais kuwa mtendaji mkuu wa NDC Dkt Shombe alikuwa anashika nafasi ya Kamishina wa Mipango ya Kitaifa kwenye Wizara ya Fedha na Mipango.