Shirika
la Taifa la Maendeleo (NDC), kupitia kiwanda chake cha Tanzania Biotech
Products Limited (TBPL), cha Kibaha - Pwani, kipo mbioni kuzalisha viuatilifu
vya kuangamiza wadudu dhurifu kwenye mazao pamoja na mbolea za kibaiolojia.
Hayo
yameelezwa na Mkurugenzi Mwendeshaji wa NDC, Dkt. Nicolaus Shombe wakati wa
ziara ya kikazi ya Balozi wa Cuba nchini Tanzania, Mhe. Yordenis Despaigne alipotembelea
kiwanda cha TBPL, Kibaha.
Dkt.
Shombe ameeleza kuwa NDC kupitia kiwanda chake cha TBPL wameshaanza kuzalisha
viuatilifu vya majaribio na matokeo ni mazuri hasa katika zao la pamba.
“Tumeshafanya
majaribio na taasisi mbalimbali za tafiti pamoja na Wizara ya Kilimo na matokeo
ni mazuri,” ameeleza Dkt. Shombe.
Dkt.
Shombe amesema uzalishaji wa viuatilifu na mbolea utaliongezea Taifa kipato kwa
kupunguza uagizwaji wa bidhaa hizo nje ya nchi na itasaidia kuongeza mnyororo
wa thamani kuanzia uzalishwaji wa bidhaa hizo mpaka kumfikia mtumiaji.
Nae
Balozi wa Cuba nchini Tanzania, Mhe. Yordenis Despaigne amesema ana imani
uzalishaji wa viuatilifu na mbolea utaanza mapema na kuleta tija kwa nchi hasa
kwenye sekta ya kilimo.
Balozi
Despaigne amesema kuwa wapo tayari kutoa msaada wa kiufundi kwa TBPL ili
kuzalisha bidhaa zenye ubora. “Timu yetu ya wataalam imeshafika na kesho
tunatarajia kuanza majadiliano na NDC,” ameeleza Balozi Despaigne.