
Tanzania
inatarajiwa kuzalisha matairi milioni 20 kwa mwaka ifikapo mwaka 2023, hayo
yamesemwa leo na Capt. Amri Said wakati wa utiaji sahihi Mkataba wa Upangaji wa
eneo la Uwekezaji la KMTC kati ya Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) na kampuni
ya Sayinvest Overseas Limited, shughuli iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano
wa NDC, Posta jijini Dar es Salaam.
Utiaji
huo wa sahihi umehudhuriwa na Menejimenti ya NDC ikiongozwa na Mkurugenzi Mwendeshaji,
Prof. Damian Gabagambi Pamoja na wawakilishi wa Sayinvest Overseas Limited
wakiongozwa na mmiliki wake Capt. Amri Said.
Kiwanda
hicho kinachotarajiwa kuzalisha matairi kati ya milioni 15 hadi 20 kwa mwaka kitafahamika
kama General Tyre Tanzania Limited, kikiwa chini ya kampuni ya Kitanzania ya Sayinvest
Overseas Limited na kitajengwa kwenye eneo Maalum la Uwekezaji la KMTC linalomilikiwa
na NDC, lenye ukubwa wa Hekta 229.13 lililopo Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro.
Uanzishwaji
wa kiwanda hiki utaambatana na uwekezaji wa teknolojia ya kisasa ambayo itachochea
uzalishaji wa magurudumu imara na yenye ubora wa hali ya juu ambayo yataleta
ushindani katika soko la dunia.
Shughuli
za ujenzi wa kiwanda zinatarajiwa kuanza mwezi mmoja mara baada ya kutia sahihi
Mkataba wa Upangaji ambapo NDC ndio mpangishaji wa eneo hilo.
Awamu
ya kwanza itahusisha ujenzi wa miundombinu na ufungaji wa mitambo pamoja na
vifaa vingine vinavyohusika huku awamu ya pili ikichukua mwaka mmoja
kukamilika.
Inatarajiwa
kuwa ndani ya miaka 3 kiwanda kitaanza uzalishaji rasmi na kitachochea ukuaji
wa uchumi na kuongeza ajira kwa Watanzania ambapo itapunguza uagizwaji wa magurudumu
ya magari kutoka nje ya nchi hivyo kuchochea biashara za ndani, kwani malighafi
itakayotumika kuzalisha magurudumu hayo itatoka hapahapa nchini katika mashamba
ya mpira yanayomilikiwa na NDC yaliyopo Tanga na Morogoro.
Shirika
la Taifa la Maendeleo (NDC) ni taasisi inayo chochea na kuongoza Maendeleo ya Viwanda
iliyoanzishwa mwaka 1962, ikijulikana kama Shirika la Maendeleo Tanganyika
(TDC) kwa Sheria ya Bunge ili kufadhili miradi muhimu ya kimaendeleo na
kuchukua nafasi ya Shirika la Kikoloni la Maendeleo (CDC) lililo anzishwa mwaka
1947/1948.