NDC kuifanya Mara kuwa ya mfano kutokomeza Malaria

Tunataka ifike mahali tuseme tumepambana na kuua mbu kwa dawa iliyo tengenezwa na kiwanda kinacho simamiwa na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), kwani kinga ni bora kuliko tiba.

Hayo yamesemwa leo na Mkuu wa Mkoa wa Mara, Mh. Adam Malima pindi akipokea lita 3,885 za viuadudu vya kuangamiza mazalia ya mbu vyenye thamani ya shilingi milioni 52 za Kitanzania, kutoka Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) kupitia kiwanda chake cha Tanzania Biotech Products Limited (TBPL), cha mkoani Pwani, wakati wa hafla fupi ya makabidhiano iliyofanyika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara.

Alisisitiza kuwa, lengo lao ni kuona mkoa wa Mara unakua wa mfano katika harakati za kupambana na Malaria, si Mara tu bali Tanzania kwa ujumla ili ulimwengu mzima uje kujifunza mbinu iliyotumiwa na Tanzania kupambana na ugonjwa huo.

Alikishukuru kiwanda (TBPL) kwa utayari wao wa kuwakopesha viuadudu hivyo, lakini mahitaji yao hasa ni lita elfu 20 ambazo ameahidi ndani ya miezi michache wataagiza tena ili kuhakikisha zoezi hilo linakua endelevu na kuhakikisha mkoa wa Mara unakua mkoa wa mfano ndani na nje ya mipaka ya Tanzania.

Kwa kutia mkazi alisema kuwa, ana amini njia ya kutumia viuadudu ina ufanisi mkubwa kuliko njia nyingine kwani nchi zilizo tokomeza kabisa ugonjwa wa Malaria walitumia njia hii, hivyo yeye ni muumini mkubwa wa viuadudu. “Watanzania tutambue, njia hii ina tija kuliko njia nyingine,” amesema Malima.

Aliendelea kueleza, matumizi ya viuadudu yanapaswa yatengenezewe mpango wa kitaifa ili Tanzania ipambane ipasavyo na Malaria kwani kwa mkoa wake huu ni mwaka wa 3 mfululizo wamekua wakipambana kufanya mkoa wa Mara utambulike kwa mambo mazuri ikiwemo kutokomeza kabisa Malaria. “Tunataka mkoa wetu utambulike kwa mambo mazuri ikiwemo kutokomeza Malaria kwa kutumia viuadudu,” amesema Malima.

Kwa kulipa uzito suala hilo alieleza kuwa watakwenda Wizarani ili waombe kuwekewa bajeti ya viuadudu kwani ana amini kinga ni bora kuliko tiba na kuwasihi Waratibu wa Malaria kufuata masharti ya dawa ili kuhakikisha wanafikia lengo la kupambana na ugonjwa huo, “tunataka kuona Malaria imeshuka misimu yote ya mwaka,” alisisitiza.

Nae Mratibu wa Malaria mkoa wa Mara, Daktari Damian Masolwa alimpongeza Mkuu wa Mkoa wa Mara kwa uzalendo wake wa kuamini matumizi ya viuadudu kuwa ni njia sahihi na ameahidi mkoa wa Mara utakua mkoa wa mfano katika kutokomeza Malaria. “Nitasimamia hili zoezi kwa ukaribu zaidi na nina imani tutatokomeza Malaria,” amesema Masolwa.

Aliendelea kueleza kuwa mkoa wake bado una kiwango kikubwa cha Malaria ila ana amini ujio wa dawa hizo utapunguza kabisa kiwango cha Malaria.

Kwa kuonesha ufanisi wa viuadudu hivi, Afisa Mhamasishaji kutoka Taasisi isiyo ya Kiserikali ya Kumekucha Tanzania, wanao shirikiana na NDC katika kutoa elimu na kuhamasisha matumizi ya viuadudu, Charlotte Nziku alieleza kuwa viuadudu hivyo vipo vya aina mbili, vile vinavyo wekwa kwenye maji machafu (Gliselesf) na kwenye maji masafi (Bactivec) na havina madhara kwa binadamu na viumbe wengine kwani vinalenga kumuangamiza kiluwiluwi wa mbu pekee.

Aliendelea kusisitiza kuwa Watanzania waone fursa katika viuadudu hivi kwani wanaweza kuwa mawakala na kurahisisha upatikanaji wa viuadudu hivi kwa urahisi kuliko kutegemea kufuata kiwandani.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mwendeshaji wa NDC, Prof. Damian Gabagambi, Mkurugenzi wa Fedha wa NDC, Rhobi Sattima alimshukuru Mkuu wa Mkoa wa Mara, Mh. Adam Malima kwa utayari na uzalendo wake wa kununua viadudu hivyo, pia alimpongeza kwa moyo wake wa kujali afya za wananchi wake kwa kuamua kuunga mkono juhudi za kutokomeza Malaria.

Akiupongeza mkoa wa Mara kwa jitihada zake za kupambana na Malaria, Rhobi Sattima alitoa rai kwa mikoa mingine kuunga juhudi za kupambana na ugonjwa huu. “kiwanda chetu kina uwezo mkubwa wa kuzalisha dawa,” alieleza.

Alisema, lita 3,885 walizo toa ni mwanzo tu kwani wataleta nyingine kama Mkuu wa Mkoa alivyo eleza na amesema zoezi hilo limeshafanyika katika mikoa ya Mbeya, Songwe na Mwanza na mipango yao ni kufika nchi nzima. “Tutaendelea na zoezi hili kwani uwezo tunao,” alisisitiza Rhobi Sattima.

Inatarajiwa kuwa lita hizo 3,885 zitagawanywa katika Wilaya zote za mkoa wa Mara wenye ukubwa wa Kilomita za Mraba 21,760, ikiwemo Wilaya ya Bunda, Butiama, Musoma Vijijini, Musoma Mjini, Rorya, Serengeti na Tarime.

Ikumbukwe kiwanda hiki cha kuzalisha viuadudu mahususi kwa ajili ya kuangamiza mazalia ya mbu, Tanzania Biotech Products Limited (TBPL), kilizinduliwa ramsi na Rais wa Awamu ya 4 Mh. Dkt. Jakaya M. Kikwete pamoja na Waziri Mkuu wa Ethiopia Hailemariam Desalegn, 2 Julai 2015 Kibaha, Pwani.