NDC KUSHIRIKIANA NA TEMDO KUBUNI NA KUTENGENEZA MASHINE NA VIFAA TIBA

Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) linatarajia kushirikiana na Taasisi ya Uhandisi na Usanifu wa Mitambo Tanzania (TEMDO) katika kubuni na kuzalisha mitambo mbalimbali ya viwanda pamoja na vifaa ikiwemo vifaa tiba.

Haya yamebainishwa katika ziara maalum yenye lengo la kujifunza pamoja na kuangalia maeneo ambayo NDC inaweza ikashirikiana na TEMDO iliyofanywa na Menejimenti ya Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) ya kutembelea makao Makuu ya TEMDO yaliyopo Njiro jijini Arusha.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo NDC, Mratibu wa ziara hiyo ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti na Mipango NDC, Dk Grace Aloyce amesema lengo la ziara hiyo ni kuangalia namna ambavyo NDC inaweza ikashirikiana na TEMDO katika kuendeleza sekta ya viwanda kwa kuwa taasisi zote zinahusika moja kwa moja katika maendeleo ya kukuza na kuendeleza sekta ya viwanda hapa nchini.

’Tumeamua kuja hapa TEMDO hasa kujifunza lakini pia kuja na mikakati ya namna ambavyo NDC na TEMDO zinaweza zikakaa pamoja na kuainisha maeneo ambayo tunaweza kushirikiana kiteknolojia pamoja na katika hatua nzima ya uzalishaji wa vifaa mbalimbali” alisema Dk Grace.

Dk Grace pia alitumia fursa hiyo kuifahamisha Menejimenti ya TEMDO juu ya namna ambavyo wanaweza wakashirikiana na NDC katika kutumia kiwanda cha KMTC Mashine Tools LTD kinachomilikiwa na NDC kilichoko Moshi mkoani Kilimanjaro katika kuzalisha vifaa mbalimbali mathalani uzalishaji wa vifaa tiba ikiwa ni moja kati ya mpango ambao uko mbioni kutekelezwa na TEMDO kwa kuwa kiwanda hicho kina uwezo na teknolojia ya kuzalisha vifaa hivyo.

Ikiwa ni adhima ya Serikali ya kukiboresha kiwanda cha KMTC Dk Grace alibainishwa kuwa Serikali kwa hivi sasa iko katika mchakato wa ujenzi wa tanuru la kuyeyushia chuma (Foundry) ambapo ujenzi wa mitambo maalum ya kuzuia kutu (Galvanising) ukiwa tayari umekamilika kwa asilimia 98.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa TEMDO Mwandisi Elisante  Mjema akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TEMDO, amesema wamekuwa wakishirikiana na NDC katika maeneo mbalimbali lakini ziara ya leo itafungua fursa zaidi za nyanja za ushirikiano baina ya taasisi hizi mbili mathalani katika mahitaji ya TEMDO kutaka kutumia kiwanda cha KMTC katika uzalishaji wa vifaa mbalimbali ni makubwa mno.

“TEMDO ina wabunifu,wasanifu na ina uwezo mkubwa wa kubuni vitu mbalimbali vya kumsaidia Mwananchi ili linapokuja suala la kuzalisha kwa wingi tunashindwa kwa kuwa hatuna uwezo huo lakini kiwanda kama KMTC kinaweza kuwa ni msaada mkubwa kwetu hasa pale tuanapofikia katika hatua ya uzalishaji wa wingi wa Bidhaa (Mass Production)” alisisitiza Mhandisi  Elisante.

Katika ziara hiyo Menejimenti ya Shirika la Taifa la Maendeleo NDC ilipata fursa ya kuona ubunifu wa teknolojia mbalimbali pamoja na miradi inayotekelezwa na TEMDO ikiwemo mradi ya uongezaji wa samani ya zao la Muhogo, Mradi wa utengenezaji wa vifaa tiba pamoja na majokofu ya kuhifadhia miili katika hospitali mbalimbali hapa nchini.