NDC na mchango katika Tanzania ya Uchumi wa Kati

Wakati wetu ni sasa: Sisi ni NDC mpya

Mnamo Julai Mosi 2020, Benki ya Dunia ilichapisha ripoti iliyo onesha kuwa Tanzania imeingia  katika nchi ya Uchumi wa Kipato cha Kati, hiyo ilikuwa ni hatua kubwa kwa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Rais, Mh. Dkt. John Pombe Magufuli na kwa taifa kwani ilivuka malengo iliyojiwekea ya kufika Uchumi wa Kati ifikapo mwaka 2025.

Miongoni mwa sababu zilizopelekea Tanzania kuingia katika nchi ya Uchumi wa Kipato cha Kati inatajwa kuwa ni utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati iliyobuni ajira kwa Watanzania wengi.

kwa mujibu wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, (2025) ukurasa wa 2, kipengele (1.2) inasema ”Uchumi wa kipato cha kati umehusishwa na kuwa na nchi ambayo umaskini unapunguauchumi imara unaojengwa na kuimarika kwa uzalishaji viwandani unaimarika na wananchi wanapata maendeleo.

Ili kuhakikisha taifa linaendelea kukuza uchumi wake na kufikia malengo makubwa zaidi, Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) limeona ni busara kuwanoa wafanyakazi wake katika Nyanja ya Uwekezaji hasa katika sheria ya Uanzishwaji na Usimamizi wa Miradi kwa Njia ya Ubia baina ya Serikali na Sekta Binafsi (Public Private Partnership) ili kuendana na kasi ya Serikali katika kuhimiza uwekezaji na ukuaji wa pato la taifa na la mtu mmoja mmoja kwani NDC ni miongoni mwa taasisi zinazo tekeleza miradi ya kimkakati inayobuni ajira kwa watanzania wengi wa vipato tofauti tofauti.

Kwa siku mbili mfululizo kuanzia tarehe 22.07.2020 hadi 23.07.2020, wakufunzi kutoka Wizara ya Fedha na Mipango wakiongiozwa na Dr. John Mboya wameendesha Semina Elekezi kwa baadhi ya wafanyakazi wa NDC wakiongozwa na Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika, Prof. Damian Gabagambi, ili kuwajengea uwezo utakaowasaidia kulinufaisha taifa kupitia rasilimali zake.

Semina hiyo iliyofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa NDC, jijini Dar es Salaam ilihusu Masuala ya Uanzishwaji na Usimamizi wa Miradi kwa Njia ya Ubia baina ya Serikali na Sekta Binafsi (Public Private Partnership) na ilijikita hasa katika Sheria ya Ubia baina ya Serikali na Sekta Binafsi (Public Private Partnership Act) ya  mwaka 2010 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2017.

NDC ikiwa ni mkono wa Serikali katika uwekezaji, ina miradi kadha wa kadha katika sekta mbalimbali kama; kilimo, Afya, Madini, na Nishati, hivyo mafunzo haya yalilenga kuwawezesha wafanyakazi kuelewa sheria na miongozo ya ubia baina ya Serikali na Sekta Binafsi.

Kulingana na kifungu cha 4 (5) cha Sheria ya Uanzishwaji na Usimamizi wa Miradi kwa Njia ya Ubia baina ya Serikali na Sekta Binafsi (Public Private Partnership) ya mwaka 2010 iliyofanyiwa marekebisho 2017 ina ainisha sekta kadha wa kadha zinazo angukia katika Ubia baina ya Serikali na Sekta binafsi kama; Kilimo, Miundombinu, Viwanda, Madini, Afya, elimu, Mazingira, Biashara na Uwekezaji, hivyo Shirika halikuwa na budi kuwawezesha wafanyakazi wake kuelewa namna ya kutengeneza mazingira bora ya uwekezaji kwa kuvutia uwekezaji, kukabiliana na changamoto mbalimbali na jinsi ya kuzitatua ili kusaidia taifa kunufaika na rasilimali zake.

Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) ni taasisi inayo chochea na kuongoza Maendeleo ya Viwanda iliyoanzishwa mwaka 1962, ikijulikana kama Shirika la Maendeleo Tanganyika (TDC) kwa Sheria ya Bunge ili kufadhili miradi muhimu ya kimaendeleo na kuchukua nafasi ya Shirika la Kikoloni la Maendeleo (CDC) lililo anzishwa mwaka 1947/1948.