NIMERIDHISHWA NA JITIHADA ZA NDC KUENDELEZA KILIMO CHA MPIRA

Katibu Mkuu Wizara ya Uwekezaji Viwanda na Biashara, Dkt. Hashil Abdallah ameonesha kuridhishwa na hatua inayofanywa na Shirika la Taifa la Maendeleo, (NDC), katika kuendeleza na kukuza kilimo cha zao la mpira hapa nchini.

Katibu Mkuu Wizara ya Uwekezaji Viwanda na Biashara ameyasema haya katika muendelezo wa ziara zake mara baada ya kufanya ziara maalum ya kutembelea na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa katika Shamba la Serikali la Mpira lililiko wilayani Muheza, Mkoani Tanga ambalo linalosimamiwa na kuendeshwa na NDC.

Dkt. Abdallah amesema ameridhishwa na mikakati mbalimbali inayofanywa na NDC kukuza uzalishaji wa zao hilo hapa nchini ikiwemo uandaaji wa miche kwa ajili ya kuendeleza zao hilo ambapo akiwa shambani hapo alipokea taarifa kuwa tayari kiasi cha miche ya mpira 1,500 imeshaandaliwa ili kupandwa ikiwa ni hatua inayofanywa na NDC katika kuhakikisha inaendeleza upandaji na uboreshaji wa shamba hilo hapa nchini.

"Nimefurahishwa na hatua mnazofanya za kuongeza miche kwa ajili ya kupanda miti mipya ambapo nilipotembelea Kalunga niliona kiasi cha miche laki moja na kumi elfu imeshaandaliwa tayari kwa kupandwa na hapa leo nimeambiwa mna miche 1,500 ni hatua nzuri katika kuboresha na kuongeza ukubwa wa mashamba yetu.”

Awali Mkurugenzi Mwendeshaji wa NDC, Dkt. Nicolaus Shombe akimkaribisha Katibu Mkuu alizungumzia juu ya mikakati mbalimbali inayofanywa na NDC  kuboresha shamba hilo ikiwemo kuongeza kasi ya upandaji wa miche.

Dkt. Shombe alitoa taarifa ya uvamizi ambao umekuwa ukifanywa na wananchi ambao kwa hivi sasa wamevamia sehemu ya shamba hilo kwa kufanya shughuli za kibinadamu ikiwemo shughuli za kilimo pamoja na makazi.

Kuhusiana na suala la uvamizi wa shamba hilo Dkt. Abdallah akiongea na Uongozi wa kijiji cha Kwaisaka kilichoko kata ya Tongwe wilayani Muheza ambapo shamba hilo lipo Dkt. Abdallah aliutaka Uongozi wa kijiji kupitia kwa Mwenyekiti wa kijiji hicho hicho, Hamis Rajabu Hussein kuhakikisha wanawaelimisha wananchi kuacha tabia ya kuvamia maeneo ya Serikali yaliyotengwa kwa ajili ya shughuli maalum na kuamua kuendesha shughuli zao za maisha ikiwemo kilimo pamoja na makazi kwa kuwa kufanya hivyo ni kinyume na sheria na taratibu nchi.

Dkt. Abdallah pia ametaka kufanyika kwa uhakiki wa mipaka ya kuzunguka shamba hilo hali itakayopelekea mipaka yake kujulikana na hivyo kuepusha changamoto ya wananchi kuingia eneo hilo na kuendesha shughuli zao za kilimo pamoja na makazi.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa kijiji cha Kwaisaka, Hamis Rajabu Hussein amekiri kuna tabia ya wananchi kuvamia eneo hilo na kwamba amepokea maelekezo ya Katibu Mkuu na atakuwa anawaelimisha wananchi wa kijiji hicho kuacha kuvamia na kuanzisha shuguli za kilimo na makazi katika eneo hilo kwa kuwa ni eneo maalumu lililotengwa na Serikali kwa ajili ya uzalishaji wa zao la mpira na lazima lilindwe kwa manufaa ya kizazi cha leo na cha kesho.

"Kuhusu suala la uvamini tutakuwa tuna wapa wannchi elimu na kuhakikisha hawavamii maeneo ya umma yaliyotengwa kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali.


Kaimu Mkurugenzi wa Viwanda vya Kuongeza Thamani NDC, Esther Mwaigomole (mwenye tshirt ya kijani), akimuonesha Katibu Mkuu wa Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt. Hashil Abdallah namna utomvu unavyogemwa katika shamba la mpira Kihuhwi.

Ziara ya Katibu mkuu wa Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara ni muendelezo wa ziara ambazo anazifanya katika kutembelea miradi mbalimbali ya Serikali ambapo mapema wiki iliyopita wakiwa pamoja na Waziri wa Uwekezaji Viwanda na Biashara Dkt. Ashatu Kijaji walipata fursa ya kutembelea shamba la mpira la Kalunga lililoko Kilombero mkoani Morogoro ambalo pia linamilikiwa na NDC.