NYERERE NGUZO YA MAENDELEO NDC

Uongozi wako thabiti kwenye Sekta ya Viwanda ni alama kwetu

Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) linaungana na Familia ya Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Watanzania wote katika Kumbukizi ya miaka 21 tokea kifo chake kilichotokea tarehe 14 Oktoba, 1999.

 

Uanzishwaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) uliasisiwa na Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1965 kwa tamko la Rais (The Presidential Order Number 5 of 1964) ambapo lilipewa majukumu na shughuli zilizokuwa zinafanywa na Shirika la Maendeleo la Tanganyika (TDC), ambayo yalikuwa ni kuanzisha na kuendeleza Viwanda Mama na Viwanda vya Kuongeza Thamani kwa kushirikiana na taasisi binafsi.

 

Serikali ilianzisha NDC ili kuwa na chombo cha Umma kitakacho buni, kuendeleza na kusimamia utekelezaji wa miradi ambayo inatoa mchango mkubwa katika maendeleo ya Taifa. Katika uanzishwaji wake NDC ndiyo iliyoanzisha viwanda vyote vilivyokuwa vinamilikiwa na Serikali. NDC ilikuwa Shirika Hodhi (holding corporation) la Serikali kwa makampuni na taasisi mbalimbali. Hii iliendana na mfumo wa kiuchumi wa wakati huo uliotokana na Mlengo wa Ujamaa na Kujitegemea ambapo Serikali ilimiliki njia kuu za kiuchumi, sera hii ilitokana na Azimio la Arusha la 1967.

 

Tokea uanzishwaji wake Shirika limeendelea kutekeleza miradi mbalimbali iliyoasisiwa na Baba wa Taifa na limeanzisha miradi mipya kulingana na majukumu yake. Miradi hiyo inagusa Sekta zote muhimu kama Kilimo, Madini, Afya, Viwanda, Nishati, Miundombinu na Biashara. Baadhi ya miradi hiyo ni; Migodi ya Makaa ya Mawe Mchuchuma, Ngaka na Kataweka; Chuma cha Liganga, viwanda vya kuzalisha bidhaa mbalimbali kwa kushirikiana na Sekta Binafsi.  Vilevile, Shirika linasimamia Bandari Kavu ya Nafaka - ETC Cargo, Dar es Salaam na Mashamba ya Mpira yaliyopo Morogoro na Tanga.

 

Aidha, Shirika linamiliki Maeneo ya Uwekezaji (Industrial Parks) ambayo ni; - TAMCO-Kibaha; Kange -Tanga; KMTC-Kilimanjaro na Nyanza-Mwanza. Baadhi ya maelezo ya miradi inayotekelezwa ni kama ifuatavyio:-

 

  1. KIWANDA CHA KUUNGANISHA MATREKTA AINA YA URSUS

Kiwanda hiki kipo Kibaha, Pwani na ni matokeo ya Mkataba wa Ushirikiano wa Kiuchumi baina ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Poland. Mradi ulizinduliwa rasmi tarehe 21 Juni, 2017 na Rais, Mhe. Dkt. John P. Magufuli ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015 ibara ya 85. Matrekta hayo yanauzwa kwa pesa tasilimu na kwa mkopo usiokuwa na riba wala dhamana hivyo umesaidia wananchi hasa wa kipato cha chini kumiliki matrekta na kuongeza uzalishaji. Lengo la NDC na Serikali ni “kulipeleka jembe la mkono Makumbusho. Matrekta haya pamoja na vifaa vyake bado yapo na yanauzwa kwa bei nafuu.

 

2. KIWANDA CHA KUZALISHA VIUADUDU VYA KUANGAMIZA MAZALIA YA MBU - TANZANIA BIOTECH PRODUCTS LTD (TBPL)

Kiwanda hiki kipo Kibaha, Pwani na ni cha kipekee, kwani kipo kimoja barani Afrika kikiwa kiinamilikiwa na Serikali kwa 100% chini ya NDC, huku kikizalisha Viuadudu vya kuua viluwiluwi vya mbu waenezao Malaria na magonjwa mengine Dengue, Zika, Chikungunya, Matende na Mabusha. Katika ziara yake kwenye kiwanda hicho, tarehe 22 Juni, 2017 Mhe. Rais Dkt. John P. Magufuli aliagiza, Halmashauri zote nchini zinunue dawa hizo ili kuweza kutokomeza kabisa Malaria. Kufuatia tamko hilo NDC kwa kushirikiana na Taasisi isiyo ya Kiserikali ya Kumekucha na wadau wengine inaendesha kampeni ya kuhamasisha matumizi ya viuadudu nchini. Dawa zinapatikana kwa bei nafuu

 

3. KIWANDA CHA KUZALISHA VIPURI KMTC

Kiwanda hiki kipo Moshi, Kilimanjaro na kilijengwa mwaka 1984. NDC chini ya Serikali ya Awamu ya 5, imefufua kiwanda hiki na sasa kinazalisha mashine mbalimbali zikiwemo; mashine za kusaga, kukoboa, kuranda mbao, vipuri vya matrekta, kubuni na kuunda matela ya matrekta ya tani 5 kwa ajili ya kuwarahisishia usa­ri wakulima.

 

4. MASHAMBA YA MPIRA

Shirika limeendeleza mashamba ya mpira yaliyopo Kihuwi (Tanga) na Kalunga (Morogoro) na uzalishaji umeongezeka kutoka tani 10 kwa mwezi mwaka 2015 hadi tani 30 kwa mwezi mwaka 2020, hivyo kupunguza uagizwaji wa malighafi hiyo nje ya nchi. Mashamba haya yameajiri zaidi ya Watanzania zaidi ya 278.

 

5. MRADI WA MAKAA YA MAWE NGAKA

Mradi upo katika eneo la Ngaka, Mbinga, Mkoani Ruvuma na unatekelezwa na kampuni ya TANCOAL Energy Limited ambayo ni ubia kati ya NDC na Intra Energy (Tanzania) Limited (IETL) kampuni tanzu ya Intra Enegy Limited ya Australia. Mradi huu umechochea ukuaji wa viwanda nchini kwa kuhakikisha upatikanaji wa makaa ya mawe ambayo ni chanzo cha nishati inayotumika kwenye viwanda vya saruji na viwanda vinavyo zalisha bidhaa mbalimbali ndani na nje ya nchi kama Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi na Zambia.

 

6. MRADI WA MAGADI-SODA

Mradi huu uko eneo la Engaruka, Monduli, Arusha na umelenga kuzalisha Magadi Soda ambayo yatatumika kuzalisha bidhaa mbalimbali ikiwemo rangi za nguo, vioo vinavyotumika kwenye magari na ujenzi. Mradi huu ukikamilika utaliingizia Taifa mapato

na utaokoa fedha zinazopotea kuagiza malighafi­ kutoka nje ya nchi.

 

7. MRADI WA ENEO LA VIWANDA TAMCO, KIBAHA

Katika eneo hili ukiacha kiwanda cha matrekta cha URSUS na cha Viuadudu (TPBL) ambavyo vimeelezwa mwanzoni mwa makala hii, kuna viwanda ambavyo vimejengwa katika eneo hilo na ujenzi wa vingine unaendelea. Baadhi ya viwanda katika eneo hilo ni;

 

(i)              HESTER BIOSCIENCE AFRICA

Kiwanda hiki kipo katika hatua za mwisho za ujenzi, huku kikitarajiwa kuzalisha chanjo za wanyama (Animal Vaccines) na kupunguza gharama za uagizaji wa chanjo hizo nje ya nchi. Vilevile Kiwanda kitazalisha ajira za moja kwa moja zipatazo 200 na zisizo za moja kwa moja zaidi ya 1,000.

 

 

(ii)            KIWANDA CHA GF TRUCKS VEHICLE ASSEMBLERS

Kiwanda hiki kimekamilika na kimeanza kuunganisha magari aina ya FAW Trucks na mitambo yake. Kiwanda kina uwezo wa kuzalisha magari 1,000 kwa mwaka na kimetoa ajira za moja kwa moja 150 kwenye awamu ya kwanza ya utekelezaji. kiwanda hiki kitatatua changamoto iliyopo ya kuagiza magari na mitambo mbalimbali nje ya nchi.

 

(iii)          KIWANDA CHA VIFUNGASHIO - GLOBAL PACKAGING TANZANIA LIMITED (GPTL)

Kiwanda cha vifungashio Global Packaging (T) Limited, Kilizinduliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzani Mhe. Dkt. John P. Magufuli mwezi Juni, 2017. Kiwanda hiki kinazalisha vifungashio vyenye ujazo tofauti tofauti ambavyo vinauzwa ndani na nje ya nchi, huku kikiwa kimetatua changamoto ya kuagiza vifungashio nje ya nchi na kimetengeneza ajira takribani 120,000.

 

8. ATAMIZI YA VIJANA WABUNIFU

Shirika linafanya atamizi ya vijana wenye mawazo bunifu katika Sekta ya Viwanda, lengo ni kuwajengea uwezo wawekezaji wa ndani ili wanufaike na rasilimali za nchi kwa kuwekeza kwenye viwanda vya kimkakati vya kitaifa. Kwa sasa Shirika limefanya atamizi ya vijana wabunifu kutoka kampuni ya EDOSAMA ambapo kwa kushirikiana na NDC wamefanikisha uanzishwaji wa kampuni ya Green Gold Treasury Limited ambayo inajihusisha na uongezaji wa thamani ya mazao ya misitu.

 

Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) linakumbuka mchango wa Baba wa Taifa  katika ujenzi wa Taifa, Daima utabaki ndani ya mioyo yetu.