SERIKALI INAJIVUNIA NDC KWENYE UWEKEZAJI

Wawekezaji Sekta ya Nguo milango wazi, Magari kuanza kuunganishwa mwakani

Nimefurahi kutembelea eneo hili muhimu la Mtaa wa Viwanda la TAMCO, ambapo ni eneo muhimu katika ujenzi wa viwanda.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Viwanda na Biashara, Prof. Kitila Mkumbo baada wakati wa ziara ya kutembelea Kongane ya Viwanda ya TAMCO, Kibaha mkoani Pwani inayo milikiwa na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC).

Ameeleza kuwa eneo hilo la uwekezaji la TAMCO limegawanyika kwenye maeneno makubwa matatu; eneo la ujenzi wa viwanda vya magari, ujenzi wa viwanda vya madawa na ujenzi wa viwanda vya nguo.

Prof. Mkumbo ameeleza katika katika maeneo hayo matatu, eneo kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya nguo ndio kubwa na mpango mmoja wapo wa eneo hilo ni kuona uwekezaji wa kiwanda kitakacho zalisha nguo zinazotumika kwenye Sekta ya Afya unafanyika.

“Tumeshakamilisha mpango wa eneo hili na tunakaribisha wawekezaji kwa ajili ya kuwekeza katika Sekta ya Nguo,” ameeleza Prof. Mkumbo.

Ameendelea kueleza kuwa lengo la Serikali ni kuona nguo zote zinazotumika kwenye Sekta ya Afya zinazalishwa hapahapa nchini ili kuleta tija kwenye sekta hiyo kwa kuona nguo zinazo tumika kwenye huduma za afya zinapatikana kwa urahisi na kwa wakati.

Pia akagusia eneo la ujenzi wa viwanda vya kuunganisha magari ambapo tayari kuna viwanda viwili, kiwanda cha GF Assemblers, kinacho unganisha magari aina ya FAW na kiwanda cha matrekta kinacho milikiwa na Serikali kupitia NDC.

Licha ya uwepo wa viwanda hivyo, Prof. Mkumbo ameeleza kuwa Serikali inatarajia ifikapo mwakani kuwe na uwekezaji mwingine wa kuunganisha magari katika eneo hilo.

“Tunatarajia ifikapo mwakani, magari aina ya TATA yaanze kuunganishwa kwenye eneo hili,” amesema Prof. Mkumbo.

Eneo la tatu ni kwa ajili ya ujenzi wa viwanda vya madawa ambapo kuna kiwanda cha kuzalisha dawa za kibaiolojia (viuadudu) kwa ajili ya kuangamiza mazalia ya mbu, Tanzania Biotech Products Limited (TBPL), kiwanda kinacho milikiwa na Serikali kwa 100% pamoja na kiwanda cha kuzalisha chanjo za wanyama cha Hester Bioscience Africa.

Mbali na hivyo pia kuna kiwanda cha kuzalisha vifungashio cha Global Packaging (T) Limited, kiwanda kinachomilikiwa kwa ubia baina ya Sekta Binafsi na NDC.

Nae Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), Dkt. Nicolaus Shombe ameeleza kuwa jukumu kubwa la NDC ni kuendeleza na kusimamia viwandana kwa niaba ya Serikali.  

“NDC ni mkono wa Serikali katika uwekezaji na tunaendelea kufanikisha lengo hilo kwa kusimamia ujenzi wa viwanda katika kongane hiyo ya TAMCO,” ameeleza Dkt. Shombe

Pia ameeleza kuwa uwekezaji uliofanyika katika kongane hiyo umeleta tija kwani umesaidia kwenye utengenezaji wa ajira kwa Watanzania.

Kongane ya viwanda ya TAMCO ina jumla ya viwanda 5 vikiwemo vya kuunganisha vyombo vya moto, viwanda vya madawa na kiwanda cha kuzalisha vifungashio vya mazao mmbalimbali.