
Imeelezwa kuwa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) ni mkono wa Serikali kwenye uwekezaji kwa kushirikiana na Sekta Binafis na lina nafasi kubwa ya kuchangia katika maendeleo ya sekta viwanda nchini Tanzania.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mwendeshaji wa NDC , Dkt. Nicolaus Shombe alipotembelea banda la shirika hilo kwenye Maonesho ya Bidhaa za Viwanda vya Wanawake yanayoendelea katika Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi huyo amesema kuwa NDC inawekeza katika viwanda vya msingi ambavyo vinaleta matokeo chanya kwenye viwanda vingine kupitia miradi mbalimbali inayotekelezwa na NDC ikwemo mradi wa makaa ya mawe, mpira na magadi soda imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya Sekta ya Viwanda Nchini.
" NDC tumekuwa tukiwekeza katika maeneo ya kimkakati kwa kushirikiana na sekta binafsi kwenye Viwanda ambavyo vinaleta tija katika viwanda vingine , mfano mradi wa magadi soda ndio kila kitu katika sekta ya viwanda hapa nchini " amesema Shombe
Ameongeza kuwa NDC inafanya biashara ya kuuza viuadudu vya kuangamiaza mazalia ya mbu na inauza bidhaa hiyo nje ya nchi kama vile Angola, Nigeria, Kenya, Eswatini na maeneo mengine.
Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), Dkt. Nicolaus Shombe akizungumza na waandishi wa habari alipotembelea banda la NDC, kwenye Maonesho ya Bidhaa za Viwanda vya Wanawake yanayoendelea katika Viwanja vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam.
Ameeleza kuwa lengo ni kuwa na NDC mpya ambayo italeta tija kwenye maendeleo ya uchumi wa nchi kutokana na miradi mbalimbali inayotekelezwa na shirika hilo.
Akizungumzia uwepo wa banda la NDC katika maonesho ya bidhaa za wajasiriamali mali wanawake yanayoendelea katika Viwanja amesema vya Mnazi Mmoja, jijini Dar es Salaam, Shombe amesema kuwa lengo ni kuendelea kuwashika mkono wanawake ambao wana mchango mkubwa katika shughuli za maendeleo ya Taifa.