USHIRIANO WENYE DIRA YA MAENDELEO

Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, wakiongozwa na Mwenyekiti wao Prof. Emmanuel Mjema ambaye ni Mkuu wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) wamefanya ziara katika taasisi za TEMDO, CAMARTEC, SIDO za jijini Arusha na kiwanda cha KMTC kinachomilikiwa na Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC) cha mkoani Kilimanjaro, pamoja na Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO), kwa lengo la kujifunza mambo mbalimbali yanayofanywa na taasisi hizo.

Ziara hiyo inakuja baada ya kuona uhitaji wa kufahamiana zaidi ili kuona namna bora ya kubadilishana teknolojia, ujuzi na namna bora wanayoweza kushirikiana katika ujenzi wa Tanzania ya viwanda.

“Kila taasisi ilianzishwa kwa sheria yake, ila tumeona haja ya kutafuta namna bora ya kushirikiana,” amesema Prof. Mjema. Aliendelea kueleza kuwa taasisi kama TEMDO na CAMARTEC wana bidhaa nyingi wanazo zalisha ila hazifahamiki hivyo kuna haja ya wao kusaidiana katika kutengeneza mpango mkakati wa biashara zao.

Hata hivyo taasisi hizo zimekua zikishirikiana katika nyanja mbalimbali kama uhaulishaji wa teknolojia, uliopo baina ya TIRDO na NDC, CBE na SIDO kupitia mpango wa Kaizen, CAMARTEC, TEMDO na NDC, huku TANTRADE ikihusika kufungua fursa za masoko ya bidhaa zinazo zalishwa na taasisi hizo kupitia maonesho ya kitaifa na kimataifa.

Awamu ya pili ya ziara hiyo itahusisha taasisi za BRELA, TBS, Wakala wa Vipimo, FCC, CBE pamoja na FCT.