WAWEKEZAJI WANAKARIBISHWA KUWEKEZA TAMCO, KIBAHA

Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), Dkt, Nicolaus Shombe, amesema NDC ipo tayari na imejipanga kikamilifu kupokea wawekezaji wenye nia ya kuwekeza kwenye Kongane ya Viwanda ya TAMCO iliyopo Kibaha mkoani Pwani.

Dkt. Shombe amesema haya akiwa ameambatana na Menejimenti ya Shirika na baadhi ya wafanyakazi wa NDC ambao walipata fursa ya kutembelea eneo hilo.

Dkt. Shombe amesema Serikali inaendelea na ukamilishaji wa miundombinu mbalimbali ya uwekezaji katika eneo hilo ikiwemo ujenzi wa barabara huku akiwakaribisha wawekezaji walio tayari kuwekeza kwenye sekta ya nguo na mavazi, vifaa tiba na dawa pamoja na uunganishaji wa magari na mitambo mbalimbali kuja kuwekeza kwenye kongane hiyo.

Akikazia hilo, ameeleza kuwa Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuendeleza miundombinu ya Kongane hiyo ili kujenga mazingira mazuri na salama kwa wawekezaji waliopo na kuvutia wawekezaji wengi zaidi kuja kuwekeza katika eneo hilo.

Katika ziara hiyo ambayo iltumika pia katika kutembelea viwanda mbalimbali vilivyoko katika eneo la TAMCO, Dkt. Shombe amekitaka kiwanda cha kuzalisha viuadudu vya kuangamiza viluwiluwi wa mbu, Tanzania Biotech Products Limited (TBPL), kilichopo katika eneo hilo kuhakikisha kinatanua wigo wa masoko ya viuadudu ndani na nje ya nchi ili kuongeza juhudi za kupambana na mbu waenezao Malaria na magonjwa mengine kama Zika, Dengue, Chikungunya, Matende na Mabusha.

Sambamba na hilo ameutaka uongozi wa kiwanda hicho kuhakikisha wanakamilisha taratibu zote za kuanza uzalishaji wa viuatilifu vya kupambana na wadudu wadhurifu kwenye mazao kama pamba na korosho, ili kusaidai wakulima wapate kipato na kuondoa changamoto ya mazao kuharibika shambani.

Imetolewa na Idara ya Uhusiano, NDC.