MENU

WAZIRI JAFO AZITAKA HALMASHAURI NCHINI KUTOKOMEZA MALARIA

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Dkt. Selemani Jafo amezitaka halmashauri zote nchini kununua viuadudu vya kuangamiza mazalia ya mbu ili kuondokana na ugonjwa wa malaria nchini.

Waziri Jafo ameyasema hayo wakati wa ziara yake ya kikazi kiwanda cha kuzalisha bidhaa za kibaiolojia cha Tanzania Biotech Products Limited (TBPL), kilichopo Kibaha mkoani Pwani.

Ameeleza kuwa anafahamu Halmashauri zote nchini zinatenga fungu kwa ajili ya ununuzi wa dawa, hivyo hawana budi kununua viuadudu kutoka TBPL na kuvipuliza kwenye vyanzo vya mbu na kuzitaka Halmshauri kuweka mipango sawa ili waje kununua dawa.

Pia amekitaka kiwanda hicho na Wizara ya Afya kuona namna ya kuboresha mikataba yao ili lengo la kupambana na malaria liendelee kama lilivyo kusudiwa.

Mbali na hayo, Waziri Jafo amekitaka kitengo cha Masoko cha TBPL kuongeza kasi ya upatikanaji wa viuadudu kwa mwananchi mmoja mmoja ili kufikia azima ya Serikali ya kuondokana na malaria ifikapo 2030.

Aidha kwa upande wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), ambao ndio wamiliki wa kiwanda hiki kwa niaba ya Serikali kupitia kwa Mkurugenzi Mwendeshaji wake, Dkt. Nicolaus Shombe, amemueleza Waziri Jafo kuwa TBPL ina uwezo wa kuzalisha lita milioni 6 za viuadudu kwa mwaka ambazo zinatosha kupambana na magonjwa yote yanayo enezwa na mbu ukiwemo ugonjwa wa malaria.

Mbali na hilo, Dkt. Shombe amesema kiwanda hiki kimeanza uzalishaji wa viuatilifu hai (biopesticides) ambavyo vitatumika katika mazao mbalimbali ikiwemo mbogamboga pamoja na matunda hivyo kutatua changamoto kubwa inayowakabili wakulima hivi sasa ya uwepo wa wadudu dhurifu wa mazao hapa nchini.

Kiwanda cha Tanzania Biotech Product Limited (TBPL) ni kiwanda pekee barani Afrika   ambacho huzalisha bidhaa za kibaolojia ikiwemo dawa za viuadudu vya Malaria ambavyo ni mahususi kwa ajili ya kupambana na magonjwa yaenezwayo na mbu ikiwemo ugonjwa wa Malaria,Zika na Dengue.Kiwanda hiki ni matokeo ya ushirikiano baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Serikali ya Cuba na kinauwezo wa kuzalisha zaidi ya lita milioni moja kwa mwaka.

Leave a Comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *