MENU

MRADI WA MAGADI SODA KUWEKA HISTORIA MPYA

Serikali imewataka Viongozi wa Taasisi zinazohusika na Mradi wa Kimkakati wa Magadi Soda uliopo Engaruka Wilayani Monduli Mkoani Arusha kushirikiana kwa karibu katika kukamilisha taratibu zote zinazohitajika ili Mradi huo unaotarajiwa kuongeza ajira, malighafi za viwandani, kukuza biashara na uchumi wa Taifa uanze kutekelezwa kwa wakati.

Hayo yamesemwa  Desemba, 21,2023 na Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara Dkt. Hashil Abdallah akiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha Bw. Elijah Mwandubya na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Bw. Kheri Mahimbali walipotembelea Mradi huo wa Kimkakati wa Magadi kwa lengo la kuona utekelezaji wake na kutatua changamoto mbalimbali zitakazowezesha kuanza kutekelezwa rasmi kwa mradi huo.

akizungumza mara baada ya kufanya ziara katika Mradi huo Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara, Dkt. Hashil Abdallah amesema ziara ya Makatibu Wakuu katika kuutembelea mradi huo ni ishara tosha kuwa Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuona kuwa mradi huo unaanza kutekelezwa mara moja.

Ziara hii imeshirikisha wizara tatu na jumla ya Taasisi nne na itafanya kazi kwa kushirikiana na vijiji vinne katika kujadili mambo mbalimbali yanayohusu mradi na kuanza kutekelezwa kwa mradi huu ni dhahiri kuwa utasaidia katika kuboresha maisha ya wakazi wa Engaruka na Taifa kwa ujumla, kuongeza mapato kwa Serikali na Serikali ipo tayari kuhakikisha utekelezaji wake unaanza mara moja”. Amebainisha Dkt. Abdallah

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Bw. Kheri Mahimbali amebainisha kuwa kuanza kuchimbwa kwa madini ya Magadi soda nchini kutaokoa kiasi kikubwa cha fedha ambacho kimekuwa kikitumika kuagiza Magadi soda kutoka nje ya nchi kwa ajili ya matumizi viwandani ambapo takwimu zinaonyesha kuwa Serikali hutumia kiasi cha zaidi ya shilingi Bilioni moja kwa mwaka kuagiza Magadi soda nje ya nchi kwa ajili ya matumizi ya malighafi hiyo viwandani.

Sisi kama wasimamizi wa sekta ya madini hapa nchini tunahidi kutoa ushirikiano wa kutosha kwa kuwa Magadi soda ni madini muhimu sana kwa ajili ya ustawi wa viwanda vingi hapa nchini kwa kuwa yanatumika kama malighafi na tuna viwanda ambavyo tayari vinategemea malighafi hii muhimu” amefafanua  Mahimbali.

Katika hatua nyingine Mahimbali aliwataka wakazi wa Engaruka na Watanzania kiujumla kuhakikisha wanachangamkia fursa mbalimbali zitakazojitokeza pale ambapo mradi huu utakapoanza kutekelezwa hapa nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo, (NDC) Dkt Nicolaus Shombe amebainisha kuwa NDC kama mwekezaji kwa niaba ya Serikali tayari imekamilisha hatua mabalimbali za kuelekea kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo ikiwemo kufanyika kwa upembuzi yakinifu pamoja na tathmini ya mazingira huku akiishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa namna inavyouchukulia mradi huu kwa uzito wa kipekee na nia ya dhati iliyonayo ya kutaka kutekelezwa kwa mradi huu.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Monduli Mwl. Happyness Laizer pamoja na Katibu Tawala wa Wilaya ya Monduli Muhsin Kassim wamesema wapo tayari kupokea mradi huo huku wakitoa rai kwa wananchi kuchangamikia fursa zitakazotokana na utekelezwaji wa Mradi huo.

Wakizungumza kwa niaba ya wananchi wa Engaruka Viongozi wa eneo hilo wakiwemo Diwani na Mtendaji wa Kata ya Engaruka pamoja na Wenyeviti wa Vijiji vya Engaruka juu, Engaruka chini, Irerendeni pamoja na Oldonyo Lengai wameonyeshwa kufurahishwa na hatua ya Serikali kuamua kutekeleza mradi huo utawakaowaletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii hususani katika upatikanaji wa ajira, ukuaji wa biashara na uchumi kwa ujumla.

Mradi wa Magadi soda wa Engaruka ni moja kati ya miradi kumi na saba ya kimkakati ya Serikali ambao upo chini ya Shirika la Taifa la Maendeo (NDC) ambao unaelezwa kuwa utekelezwaji wake utakuwa na manufaa makubwa kiuchumi kwa Taifa kwa kuwa utasaidia katika kutoa malighafi mbalimbali za Magadi soda kwa viwanda ndani na nje ya nchi, kutoa ajira elfu moja za moja kwa moja kwa wananachi ambapo uwekezaji wake unatarajia kugharimu kiasi cha dola za kimarekani milioni mia nne.

katika eneo linalojengwa kiwanda cha kuzalisha madini aina MAGADI SODA lililopo kata ya ENGARUKA wilayani MONDULI Mkoani ARUSHA ikiwa ni hatua za kuanza utekelezaji wa ujenzi huo unaotarajiwa kutumia zaidi ya shilingi Trilioni MOJA na kumaliza kabisa tatizo la kutegemea kuagiza madini hayo nje ya nchi.

Leave a Comment

Your email address will not be published. Required fields are marked *